Urais 2015: Pinda Asema Atafurahi CCM Wakimteua Profesa Mwandosa Kugombea Urais Iwapo Jina lake(Pinda) Litakatwa
WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda, ambaye amechukua fomu za kuomba kuwania urais kupitia CCM, amesema atakuwa tayari kumuunga mgombea yeyote atakayepitishwa na chama chake. Alisema akikosa yeye atafurahi akiteuliwa Profesa Mark Mwandosya.
Akitoa salamu kwa wanachama wa chama hicho waliofika kumdhamini katika Wilaya za Mbozi, Mbeya vijijini na Mbeya Mjini ambapo zaidi ya wanachama 6,000 walimdhamini, wakati wanaotakiwa ni 30.
Akisalimia wananchi wa Mbozi akitokea Rukwa, alisema katika Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, wamepata heshima ya kuwa na wagombea wawili ikiwa ni yeye na Profesa Mwandosya, hivyo akishinda yeye itakuwa ni mipango ya Mungu na akishinda Mwandosya pia atafurahi kwa kuwa itakuwa ni heshima kwa wananchi wa kanda hiyo.
Alisema Chama hicho ili kishinde kinahitaji upendo na mshikamano. Alisisitiza kuwa hakuna maana ya kushambuliana na kuchafuana kutokana na kuwa waliochukua fomu wote ni wana-CCM na hadi sasa hakuna mwenye uhakika wa kushinda kutokana na siri hiyo Mungu pekee kuijua.
"Anayejua hadi sasa kuwa Rais wa Tano wa Tanzania ni nani ni Mungu pekee na hivyo hakuna maana ya kushambuliana kwani tunaweza kufika mwisho wa safari wakiwa vipande vipande na hivyo kuzalisha makundi makubwa ndani ya chama ambayo yatakipa shida chama kupata ushindi wa kishindo," alisema.
Alitaka wagombea kuacha kujiaminisha ushindi kwa jambo ambalo alisema haliwezekani kwa wao kuwa na uhakika wa jambo hilo kutokana na ukweli kuwa anayejua mshindi ni Mungu peke yake.
"Wako watu hadi sasa utawasikia wanasema kuwa lazima mimi niwe mimi,lazima niwe mimi jambo ambalo si la kweli kutokana na kuwa anayejua hayo ni Mungu peke yake na hivyo wanachotakiwa kujua kwa sasa ni kuwa kazi yao ni kueleza mikakati yao badala ya kujipa uhakika wa kushinda," alisema.
No comments